Pambano Kuu

1/44

Pambano Kuu

Dibaji

Kitabu hiki, msomaji, hakikuchapishwa kutueleza kuwa kuna dhambi na taabu na dhiki katika ulimwengu huu. Hayo tunayajua sana. Kitabu hiki hakikuchapishwa kutueleza kuwa kuna pambano lisilosuluhishika kati ya giza na nuru, dhambi na haki, uovu na wema, mauti na uzima. Ndani ya mioyo yetu tunalijua pambano hili, na tunajua kuwa sisi ni wahusika na watendaji katika pambano hili. PKSw 2.1

Lakini kila mmoja wetu kwa nyakati tofauti hupata shauku ya kuelewa zaidi kuhusu pambano kuu hili. Pambano lilianzaje? Au limekuwepo wakati wote? Ni mambo gani huhusishwa katika pambano kuu hili la kutisha? Je, mimi nahusikaje katika pambano hili? Wajibu wangu ni nini? Najikuta nikiwa katika ulimwengu huu bila uchaguzi wangu. Je, jambo hili ni baya au zuri kwangu? PKSw 2.2

Ni kanuni kuu zipi huhusishwa katika pambano hili? Je, pambano litaendelea kwa muda gani? Mwisho wake utakuwaje? Je, ulimwengu utazama, kama wanasayansi wengine wanavyosema, katika vina vya usiku usiokuwa na jua, ulioganda, wa milele? Au kuna mustakabali ulio bora zaidi? PKSw 2.3

Bado swali linakuja karibu zaidi: Ni kwa jinsi gani pambano katika moyo wangu, mgogoro kati ya uchoyo unaotiririka kuingia ndani na upendo unaobubujika kwenda nje, waweza kumalizika kwa ushindi wa wema, na kumalizika milele? Biblia inasemaje? Mungu anatufundisha nini kuhusu suala hili muhimu sana? PKSw 2.4

Ni kusudi la kitabu hiki, msomaji, kuisaidia roho inayotaabika ipate suluhisho la haya maswali yote. Kimeandikwa na mtu ambaye ameonja na kutambua kuwa Mungu ni mwema, na ambaye amejua kwa kuwa karibu na Mungu na kwa kujifunza neno Lake kuwa siri ya Bwana iko kwa wale wanaomcha Mungu, na kuwa Mungu anawaonesha agano Lake. PKSw 2.5

Ili tuweze kuelewa vizuri zaidi kanuni za pambano kuu, ambapo maisha ya ulimwengu wote yanahusishwa, mwandishi ameliweka mbele yetu kwa njia ya matukio halisi ya karne ishirini za mwisho. PKSw 2.6

Kitabu kinaanza na matukio ya kuhuzunisha ya kufungwa kwa historia ya mji wa Yerusalemu, mji uliochaguliwa na Mungu, baada ya mji huo kumkataa Mtu wa Kalwari, aliyekuja kuokoa. Baada ya hapo, kwenye barabara kuu ya mataifa, kinaonesha mateso ya watoto wa Mungu katika karne za kwanza; uasi mkuu uliofuata katika kanisa Lake; mwamko wa matengenezo ulimwenguni, ambapo baadhi ya kanuni kuu za pambano zinadhihirishwa kwa uwazi; somo la kutisha la Ufaransa kuzitupilia mbali kanuni sahihi; uamsho na uinuaji wa PKSw 2.7

Maandiko, na mvuto wake safi unaookoa; mwamko wa kidini wa siku za mwisho; ufunguliwaji wa chemchemi yenye nuru ya neno la Mungu, na ufunuo wake wa ajabu wa nuru na maarifa ya kukabiliana na mlipuko wa kutisha wa kila aina ya upotoshaji wa giza. PKSw 3.1

Pambano linalotukabili sasa, pamoja na kanuni zake kuu zinazohusishwa, ambapo kila mtu anahusishwa, limeelezwa kwa usahili, uwazi, na uzito. PKSw 3.2

Mwisho wa yote, tumeelezwa kuhusu ushindi wa milele na utukufu wa wema dhidi ya uovu, ukweli dhidi ya uongo, nuru dhidi ya giza, furaha dhidi ya huzuni, tumaini dhidi ya kukata tamaa, utukufu dhidi ya aibu, uzima dhidi ya mauti, na upendo wa milele na uvumilivu dhidi ya chuki na ulipizaji kisasi. PKSw 3.3

Kuanzia toleo la kwanza (1888), likifuatiwa na sahihisho la mwandishi (1911), kitabu hiki cha ajabu kimesambazwa ulimwenguni kote kwa njia ya matoleo mengi na tafsiri nyingi. Msomaji atagundua kuwa mwandishi ameandika kwa uwazi na ujasiri, akitaja makosa na kutoa suluhisho linalotolewa na Neno la Mungu lisilokosea. Na ingawa miongo michache ya hivi karibuni imeshuhudia mabadiliko na marekebisho katika ulimwengu wa kidini na kijamii, mawazo ya msingi na matukio yajayo yaliyoelezwa katika kitabu hiki yanadumu kuwa na mguso mkubwa na mvuto wa ajabu leo. PKSw 3.4

Matoleo ya awali ya kitabu hiki yameleta roho nyingi kwa Mchungaji wa Kweli; ni ombi la Mchapishaji kuwa toleo hili liwe na matunda mengi zaidi kwa ajili ya wema wa milele. PKSw 3.5

Wachapishaji.